RAIS MAGUFULI AOMBWA KUVUNJA BARAZA LA MADIWANI ARUSHA KWA KUKOSA MAADILI.

MATANGAZO

MATANGAZO
Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Wilaya ya Arusha, Martin Muniss amemuomba Rais John Magufuli kulivunja Baraza la Madiwani la Jiji la Arusha kutokana na kukosa uadilifu na kugeuka kichaka cha siasa chafu.

Muniss alitoa ombi hilo wakati akifunga kikao cha Baraza Kuu la UVCCM Wilaya ya Arusha na kueleza kuwa Baraza la Madiwani la Jiji la Arusha limekuwa na uonevu mkubwa katika maduka ya stendi ndogo na kubwa na yaliyopo soko kuu kutokana na utaratibu uliotumika kuwa wa mashaka, baada ya baadhi ya wafanyabiashara kunyang’anywa.

Alisema baadhi ya wafanyabiashara walionyang’anywa vibanda hivyo wamehusishwa na itikadi za siasa kwa CCM, hali aliyoeleza ni ukiukwaji wa haki na ubaguzi mbaya katika taifa.

“Namuomba Rais Magufuli aiokoe Arusha, kwanza alivunje Baraza la Madiwani wa Jiji, kutokana na serikali kupoteza mapato mengi huku itikadi za siasa zikitangulizwa mbele, badala ya watu kufanya kazi za kuwatatulia matatizo wananchi,” alieleza.

Alisema Meya na Madiwani wameshindwa kusimamia ukusanyaji wa mapato ya ushuru wa magari katika baadhi ya maeneo, badala yake wanaandaa hujuma za kuipaka matope serikali ili ionekane utaratibu wa kurejesha vyanzo vya mapato kutoka kwa wazabuni kuwa hauna faida.

Alisema uwepo wa madiwani katika Jiji la Arusha hauna manufaa yoyote kwa sababu viongozi hao bila huruma, walisimamia wananchi wanaotumia Soko la Kilombero kukatiwa maji kwa zaidi ya wiki tatu, soko ambalo linahudumia nusu ya wakazi wa Arusha, hadi hapo aliyekuwa Mkuu wa Wilaya, Mrisho Gambo alipoamuru AWUSA warudishe maji.

Pia aliongeza kuwa viongozi hao wamegeuza Halmashauri ya Jiji kuwa shamba la bibi la kuvuna fedha, baada ya kujiidhinishia viwango vikubwa vya posho, ilihali wananchi wa kata ya Muriet wakikabiliwa na tatizo la ukosefu wa maji na umeme huku wananchi wakichangishwa fedha za kujenga barabara yao.

HabariLeo