Mama Rwakatare awatoa wafungwa 12 gereza la Keko

MATANGAZO

MATANGAZO


Mchungaji wa kanisa la Mikocheni B Assemblies of God, Askofu Dr Getrude Rwakatare, amewatoa wafungwa 12 waliokuwa wamefungwa kwenye gereza la Keko jijini Dar es Salaam huku lengo ni kuwatoa wafungwa 78 waliofungwa kwa kukosa kulipa faini.

Akizungumza na wanahabari, Askofu Rwakatare alisema kuwa amewatoa wafungwa wanaodaiwa kiasi kidogo cha fedha na wenye makosa madogo ili waweze kurejea uraiani na kujenga taifa kwani kuendelea kuishi huko wanapoteza nguvu kazi ya kesho.

“Nipo gereza la Keko ambapo nina furaha kuwatoa wafungwa ambao wamefungwa mahali hapa kwasababu mbalimbali. Wengine wameshindwa faini ya shilingi elfu 40, wengine wameshindwa faini ya shilingi elfu 50 na wengine kukosa faini za laki moja,” alisema. “Mimi nimeguswa kama mtumishi wa Mungu na mchungaji wa mlima wa moto nikasema hapana haiwezekani wacha kile ambacho tunaweza kukifanya tukifanye kwahiyo katika gereza hili tunawatoa wafungwa 12 na tumewalipia na wamewekwa huru, mnarudi uraiani na mimi nimewaambia kwamba wawe raia wema, gerezani sio hoteli,” aliongeza.


“Wanaporudi wawe wananchi bora, mimi siwajui wengine wanatoka Mkuranga, wengine Kisarawe, wengine Temeke, wengine Ilala, kama vile tunavyoenda mahospitalini pia tuelekeze nguvu zetu magerezani kweli watu ni wahalifu lakini wanahitaji dawa vitu vidogo vidogo kama hivi watoto wadogo wapo pale wanahitaji dawa hata ya kikohozi. Tuje tusaidie sio mbaya. Unamtumikia Mungu na pia nawaasa ndugu, jamaa na ninyi wake mliorudishiwa waume zenu jamani watunzeni, watunzeni waangalieni na muwaonye,wazee kaeni na vijana waonyeni waache mambo mabaya,kwasababu wengine kweli wana makosa na wengine hawana makosa,wale wenye makosa waache uovu,hawatarudi tena mahali hapa, alisisitiza.

Baada ya Keke, Mama Rwakatare ataelekea katika gereza la Ukonga kwa ajili ya kuendelea na shughuli hiyo na amesema jumla ya kuwatoa wafungwa hao ni shilingi milioni 25 na kwamba ameguswa yeye kama mtumishi wa Mungu na kuwataka wanaotoka wawe wananchi bora na wakarudishe nguvu kazi zao nyumbani.

“Tunasema turudishe nguvu kazi inayoliliwa nyumbani wakakae na wake zao na watoto wao kwahiyo wakirudi watazalisha watafanya mambo yao, hatutetei maovu, kurudisha pia kupunguza mlolongo wa wafungwa magerezani.”