Mwijage: Serikali Haikurupuki Kufanya Maamuzi

MATANGAZO

MATANGAZO
Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhe. Charles Mwijage amefunguka na kudai serikali ya awamu ya tano huwa haikurupuki katika kufanya mambo yake kama baadhi ya watu wanavyoendelea kufikilia bali wanafanya mipango yao kwa kufuata dira na sera.

Waziri Mwijage ametoa kauli hiyo leo (Aprili 06, 2018) kwenye mkutano wa 11 unaoendelea kufanyika mkoani Dodoma wakati akijibu swali la mbunge wa Momba Mhe. David Silinde ambaye aliishauri serikali ibadilishe kauli mbio yake ya kujenga viwanda na kuiita serikali ya kuwezesha mazingira wezeshi kama baadhi ya viongozi wanavyoendelea kunadi.

"Jambo linalofanywa na serikali ya awamu ya tano sio la kuamka tu na kufanya, tunafuata dira ya 2025, tunafuata mpango wa pili wa miaka 5 na tunafuata maelekezo ya Mhe. Rais Magufuli. 
"Serikali jukumu lake ni kuweka mazingira wezeshi na kazi ya sekta binafsi ni kujenga viwanda. Sasa sisi serikali ya awamu ya tano tunajenga viwanda, sisi na sekta binafsi tunakwenda pamoja. Huwezi kutenganisha serikali na sekta binafsi",amesema Mwijage.

Pamoja na hayo, Waziri Mwijage ameendelea kwa kusema "Mhe. Silinde rafiki yangu usisahau, umeme wa Momba kama sio serikali na mimi wakati nilivyokuwa Naibu waziri wa Nishati usingeweza kufika sasa unapaswa kushukuru kwa kitego unachokipata ili tuje tukupatie kingine".

Kwa upande mwingine, Naibu Waziri, Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhandisi Stella Manyanya amewaomba wananchi wa Tanzania wasitishike katika kuanzisha viwanda nchini vinavyowezekana kulingana na mahitaji ya maeneo yao.