Serikali Yakataa Kuongeza fedha za kujikimu kwa Wanafunzi wa Vyuo Vikuu Wanaopatiwa mikopo

MATANGAZO

MATANGAZO
Serikali imekataa kuongeza fedha za kujikimu kwa wanafunzi wa elimu ya juu wanaopatiwa mikopo na Serikali kutoka Sh8,500 hadi kufikia Sh10,000 kwa siku.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Stella Manyanya amelieleza Bunge kuwa kiwango hicho kitaendelea hadi utakapofanyika utafiti baada ya miaka miwili.

Manyanya alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum,  Zainabu Katimba (CCM), aliyetaka kujua kama Serikali itakuwa tayari kuongeza fedha kwa wanafunzi hadi kufikia Sh 10,000 kwa madai gharama za maisha zimepanda.

Amesema bodi ya mikopo ilifanya ongezeko la fedha za kujikimu kwa wanafunzi wa vyuo vikuu kwa Sh1,000 kutoka Sh7,500 hadi kufikia 8,500 katika mwaka 2015/16.

“Ongezeko hilo haliendani na kasi ya mfumuko wa bei uliorekodiwa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) kutoka asilimia 4.2 Februari 2015 hadi kufikia asilimia 5.6 Februari 2016,” amesema Katimba.

Naibu waziri amesema Serikali imekuwa ikifanya utafiti wa gharama halisi za maisha kwa wanafunzi ambazo hujumuisha malazi na chakula.

Amesema katika mwaka wa fedha wa 2014/15 Serikali kupitia bodi hiyo ilifanya utafiti katika vyuo vyote nchini ili kujua gharama halisi za chakula na malazi na kuonyesha kuwa gharama halisi ilikuwa ni kati ya Sh8,000 hadi 8,500.

Naibu waziri amesema wizara itafanya utafiti mwingine ili kubaini gharama halisi za chakula na malazi kwa wanafunzi hao na matokeo yake yatatumika kupanga viwango vya fedha zitazolipwa kwa wanafunzi.