Waziri Mwakyembe Awaasa Watanzania Kupambana Na Viashiria Vinavyo Sababisha Mauaji Ya Kimbari

Na: Mwandishi wetu
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dkt Harrison Mwakyembe, amewaasa Watanzania kuhakikisha wanapambana na viashiria vyote vinavyoweza kusababisha uvunjifu wa amani na mauaji ya kimbari. Kauli hiyo  Dkt. Mwakyembe ameitoa wakati wa maadhimisho ya kumbukumbu za mauaji ya kimbari yaliyotokea nchini Rwanda miaka 24 iliyopita.

Kwenye hotuba yake Dkt. Mwakyembe amesema mauaji ya kimbari hayatokei ghafla bali huanza kwa chokochoko na kauli za kichochezi ambazo zina lengo la kuigawa jamii vipande vipande. 
“Kilichotokea Rwanda ni fundisho kwetu, mauaji ya kimbari hayatakiwi kutokea tena. Kuhakikisha hayatokei lazima tuyadhibiti mambo yote yanayoweza kuligawa taifa kwa faida ya kizazi cha leo, kesho na keshokutwa” Dkt. Mwakyembe alisisitiza.

Kuendelea kutia mkazo wa ujumbe wake Dkt. Mwakyembe aliinukuu kauli ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli, aliyoitoa wakati wa ziara yake ya kikazi nchini Rwanda  ambapo alisema “haya hayatatokea tena, hatuwezi kubadili kilichotokea awali, lakini tunaweza kubadilisha hali ya leo na hata ya baadae”.

Balozi wa Rwanda nchini mheshimiwa Eugine Kayihura ameishukuru Serikali na wananchi wa Tanzania kwa kuendelea kuwa pamoja na Wanyarwanda. Pia ameahidi kuendeleza ushirikiano wa kindugu kati ya Tanzania na Rwanda kwa maendeleo ya watu wake.

Kwa upande wake Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa, Alvaro Rodriguez amesema nchi zote zina wajibu wa kuwalinda wananchi wake dhidi ya mauaji ya kimbari, uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya binadamu. Pia zinatakiwa kuhakikisha zinaungana kupambana na mtu au kikundi chochote chenye nia ya kutekeleza uhalifu kama huo.

Kumbukumbu za mauaji ya kimbari ya Rwanda huadhimishwa kila mwaka na mwaka huu maadhimisho hayo kwa Tanzania yamefanyika ukumbi wa mikutano wa Mlimani City ambapo Dkt. Mwakyembe alikuwa mgeni rasmi. Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na wageni waalikwa mbalimbali wakiwemo mabalozi wanaowakilisha nchi zao hapa nchini, watu mashuhuri, viongozi wa serikali na mashirika ya kimataifa na wanafunzi wa shule za sekondari za jijini Dar-es-salaam
Read More

Picha: Rais Magufuli Akiwa katika Ibada ya Kumsimika Askofu Jimbo la Katoliki la Arusha

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameshiriki katika Ibada ya kumsimika Mhashamu Isaack Amani kuwa Askofu Mkuu Jimbo la Katoliki la Arusha katika Kanisa la Mtakatifu Theresia la Mtoto Yesu Jimbo Kuu Katoliki jijini Arusha leo April 8, 2018.
Read More

BREAKING: Mhariri wa Gazeti la The Guardian aokotwa Bunju akiwa hajitambui

 Mmoja wa wahariri waandamizi wa gazeti la The Guardian, Finnigan Simbeye ameokotwa eneo la Bunju wilayani Kinondoni akiwa hajitambui.

Taarifa zilizosambaa leo Jumapili Aprili 8, 2018  zinazoonyesha kitambulisho chake cha kazi cha kampuni ya The Guardian Limited zinaeleza Simbeye aliokotwa akiwa kwenye hali mbaya.

Hata hivyo, kamanda wa polisi Mkoa wa Kinondoni, Murilo Jumanne amesema hana taarifa za tukio la kuokotwa Simbeye.

Rose Mirondo, ambaye ni mkewe Simbeye amesema mumewe aliondoka nyumbani jana Jumamosi Aprili 7, 2018 akiwa na gari lakini hakurudi hadi alipopata taarifa za kuokotwa kwake leo.

Amesema alipokwenda eneo la tukio Bunju hakuliona gari la mumewe.

Rose amesema watu aliowakuta eneo la tukio wamemweleza kwamba Simbeye alichukuliwa na polisi kupelekwa hospitali.

Amesema bado hana taarifa ya hospitali gani amepelekwa na kwamba, anakwenda Kituo cha Polisi Bunju kupata taarifa zaidi.
Read More

Meya aliyesifiwa na Rais afunguka kuhusu kuhama


Meya, Wajiji la Arusha, Kalista Lazaro (CHADEMA) amefunguka na kusema kitendo cha Rais kumsifia mbele ya hadhara ni heshima kwake na viongozi wa Arusha na kusema hakuna sababu kiongozi aliyechaguliwa na wananchi kuhama chama kwa kumuunga mkono Rais.

Kalista Lazaro alisema hayo April 7, 2018 baada ya Rais Magufuli kumsifia kuwa ni kati ya watu ambao wanapenda maendeleo na kufanya maendeleo katika jiji la Arusha Mjini licha ya kiongozi huyo kutokea katika chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).

"Hii pongezi ya Rais ni kwa sababu alipokea taarifa ya utendaji ya jiji la Arusha na tangu alipoingia nilimweleza mambo ambayo tumefanya kwa mfano amepongeza jitihada kubwa ya ujenzi wa madarasa tangu mwaka 2016 ambapo tumejenga madarasa 105, 2017 tumejenga madarasa 61
"Tunapandisha vituo vya afya mara moja na dispensary kwa ujumla tano, hospitali ya wilaya, barabara za lami, barabara za vumbi na juzi tumetangaza tenda ya kilometa 10 za lami katika jiji la Arusha ambapo barabara ya Njiro, Kwa Mlombo, Sombetini zinaenda kujengwa lami pamoja na barabara ya Ngarenalo kwangu mimi ni heshima na hii heshima nimeipokea kwa niamba ya wananchi wa jiji la Arusha" alisema Kalista Lazaro

Aidha Kalista Lazaro amedai kupongezwa kwake kuwe funzo kwa viongozi wengine ambao wamekuwa wakihama kutoka CHADEMA na kwenda CCM kwa kigezo cha kuunga mkono serikali na kudai kuwa ukitaka kufanya hivyo unachotakiwa kutekeleza tu yale uliyoahidi kwa wananchi wako na si kwa kigezo cha kuhama chama.

"Wale ambao walikuwa wanabeza na hawatambui sasa wametambua kuwa Meya wao anapongezwa na Rais Magufuli mbele ya halaiki ya watu, mbele ya polisi, mbele ya Mkuu wa Majeshi hivyo Rais anaona kazi tunayofanya na niwaambie wananchi hakuna sababu ya kiongozi wa kuchaguliwa kuhama, ukitaka kutekeleza wajibu wako na kuunga mkono serikali unatakiwa ufanye kazi ambayo umeahidi wananchi wako. Mimi leo napongezwa nikiwa ndani ya CHADEMA, nikiwa Meya wa CHADEMA na diwani wa CHADEMA kwangu mimi ni heshima" alisisitiza
Read More

Serikali Kuanzisha Kampeni Ya Jiongeze Tuwavushe Salama ili kupunguza vifo vya Mama na Mtoto

Rais Mstaafu Jakaya Kikwete amesema matatizo ambayo yanatokana na uzazi yapo ambayo yanaweza kuzuilika na kuhimiza wadau kushirikiana na Serikali kwa lengo la kuendelea kupunguza vifo vya mama mjazito na mtoto.

Pia ametoa pongezi kwa hatua zinazochukuliwa na Taasisi ya Childbirth Survival International(CSI) ya kuhakikisha wanatoa elimu ya afya salama ya uzazi na kushiriki kwa vitendo katika kufanikisha vifo kwa mama na mtoto vinapungua hapa nchini.

Amesema hayo jijini Dar es Salaam wakati akitoa hotuba yake kwenye Maadhimisho ya miaka mitano ya CSI na kutumia nafasi hiyo kuwapongeza waanzilishi wa taasisi hiyo Stella Mpanda na Profesa Tausi Kagasheki.

Rais mstaafu Kikwete amesema kumekuwepo na vifo ambavyo vinatokea kwa wajawazito na watoto ambao hawana hatia na kutumia nafasi hiyo kuhimiza wadau mbalimbali kushirikiana na Serikali katika kupunguza vifo hivyo.

Amesema ipo haja ya kuendelea kutolewa elimu ambayo itasaidia jamii kutambua umuhimu wa kuhudhuria kliniki kwa mama mjazito na kubwa zaidi kuendelea kutatua changamoto zilizopo kwenye eneo la afya ya uzazi na vifo. Ameelezea hatua ambazo zinachukuliwa katika kupunguza vifo vya wajawazito na watoto.

“Nimefurahi sana kuona taasisi hii imenzishwa na akina mama wa Tanzania. Stella Mpanda yeye ni mkunga na Tausi yeye ni mwanataaluma .Nifaraja sana wamama wa Tanzania kufanya jambo kubwa kama hili la kuhakikisha wanashiriki katika kupunguza vifo vya wajawazito,

“Wametoa heshima kubwa kwa nchi yetu na pia wamefanya jambo kubwa kwa wanawake nchini kwa kuanzisha taasisi kubwa kama hii ya CSI. Kwa bahati mbaya akina mama wakati mwingine mnashindwa kupongezana. Adui wa mwanamke ni mwanamke ni mwenyewe,” amesema Rais mstaafu Kikwete.

Kuhusu changamoto zilizopo kwenye afya ya uzazi na kwamba moja ya malengo ya milenia inazungumzia kupunguza vifo vya mama mjazito na watoto chini ya miaka mitano.

“Wakati naingia madarakani mwaka 2005 , vifo kwa watoto wanaokufa ilikuwa 578 kati ya vizazi hai 100,000 wanaozaliwa. Baadae tukapunguza vifo hadi watoto 432 lakini ikapanda tena hadi vifo vya watoto 556 wakati lengo la milenia ilikuwa ni watoto 191,

“Hivyo tukaamua kuweka mikaka katika kuhakikisha tunapunguza vifo hivyo,” amesema.

Hata hivyo takwimu za mwaka 2016 kwa mujibu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ni kwamba kati ya vizazi hai 100,000 wanaopoteza maisha ni 556.

Serikali kuja na Kampeni ya JIONGEZE TUWAVUSHE SALAMA
Kwa upande wa Waziri  wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Ummy Mwalimu amesema wanatarajia kuanzisha kampeni   itakayofahamika Jiongeze tuwavushe salama.

Amesema lengo la kampeni hiyo ni kuhakikisha mama mjazimto anajiongeza kwa kuhakikisha anakwenda kituo cha afya na akifika anayetoa huduma naye ajiongeze kwa kutoa huduma sahihi ambayo mtamuwezesha mjazmito kujifungua salama.

Waziri Mwalimu ametumia nafasi hiyo kuelezea hatua ambazo Serikali ya awamu ya tano inavyochukua jukumu la kuhakikisha vifo vya mama mjazito na mtoto vinapungua ambako akagusia kampeni hiyo.

“Tumeongeza bajeti ya wizara ya afya na sehemu kubwa pamoja na kuangalia dawa na vifaa tiba pamoja na miundombinu pia tumeweka nguvu katika afya ya mama na mtoto,” amesema.

Wakati huo huo Mwalinzishi na Mkurugenzi wa CSI Stella Mpanda ameelezea namna ambavyo taasisi yao imejikita katika kuhakikisha vifo vya mama mjazito na mtoto vinaungua na kufafanua kuwa wamekuwa wakitoa elimu ya uzazi.
Read More

TUCTA Nao Wataka Watumishi Darasa la 7 Warudishwe Kazini

Baraza Kuu la Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (Tucta) jana Jumamosi Aprili 7, 2018 limetoa tamko lenye mambo saba, likiwemo la kupinga uamuzi wa Serikali kuwafuta kazi watumishi wake wenye elimu ya darasa la saba.

Akisoma tamko hilo mbele ya wajumbe wa baraza kuu la Tucta katika mkutano wa baraza hilo uliofanyika mkoani Morogoro mwenyekiti wa Tucta, Tumaini Nyamhokya alisema uamuzi huo wa Serikali si sahihi na hivyo wametaka watumishi hao kurejeshwa kazini.

Alisema baraza limesikitishwa na uamuzi wa kuwaondoa kazini watumishi wa umma na taasisi zinazopokea ruzuku kutoka serikalini.

Nyamhokya alisema uamuzi huo si wa kisheria ikizingatiwa kuwa watumishi hao waliajiriwa kwa kufuata taratibu halali za ajira.

“Kwa hiyo Tucta tunaitaka serikali kutengua uamuzi wake na kuwarudisha watumishi hao kazini bila kupoteza haki zao za kiutumishi kwa kipindi chote,” alisema.

Mambo mengine sita yaliyopo katika tamko hilo wanayotaka yafanyiwe kazi ni; ongezeko la mishahara, kodi ya mishahara (PAYE), kupandishwa madaraja na vyeo kwa watumishi wa umma, malimbikizo ya mishahara kwa wafanyakazi na watumishi kwa baadhi ya taasisi, ucheleweshwaji wa malipo ya wastaafu kwa baadhi ya mifuko ya hifadhi ya jamii na uamuzi wa Serikali kuunganisha mifuko ya hifadhi ya jamii.
Read More

Viongozi wa kitaifa,Wazungumzia maendeleo yaliyoachwa na Rais wa kwanza Z'bar

Viongozi wa Kitaifa kutoka Zanzibar na Tanzania Bara wamesema Watanzania wanaendelea kumkumbuka Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Hayati Sheikh Abeid Amani Karume kutokana na Maendeleo makubwa aliyoyafanya wakati wa Uongozi wake miaka minane na kufanikiwa kuacha historia isiyofutika kwa kufanikisha Mapinduzi ya Zanzibar na tukio la kuzaliwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania April 26, mwaka 1964.

Viongozi hao wametoa kauli jhiyo jana kwa nyakati tofauti, muda mfupi baada ya kukamilika kwa shughuli ya kumbukumbu ya miaka 46 ya kifo cha Rais wa Kwanza wa Zanzibar Hayati Sheikh Abeid Amani Karume iliyofanyika katika ofisi kuu ya Chama cha Mapinduzi iliyopo Kisiwandui visiwani hapa.

Walisema yanayooneka hivi sasa Zanzibar yametokana na dira ya maendeleo iliyoachwa na Marehemu Abeid Amani Karume ya kuwaletea wananchi Maendeleo katika sekta mbalimbali kwa kuondosha matabaka na kufanikiwa kujenga umoja wa kitaifa pamoja na kuasisi Muungano ambao umevunja rekodi kwa kudumu zaidi ya miaka 50.

Kila ifikapo April 7 kila mwaka, Watanzania huadhimisha kumbukumbu ya kifo cha Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Hayati Sheikh Abeid Amani Karume ambaye aliuwawa na Wapinga Maendeleo na kuacha simanzi na majonzi kwa wanaharakati wa ukombozi wa Bara la Afrika.
Read More

Profesa Jay akumbuka msoto wa Maisha....Asimulia Alivyokuwa Anakunywa Maji ya Chooni na Kupanda Malori

Nguli wa muziki wa Bongo Fleva ambaye pia ni mbunge wa jimbo la Mikumi, Joseph ‘Profesa Jay’ Haule, amekumbuka msoto aliokutana nao wakati anatafuta kutoka kimuziki miaka ya 1990 akiwa na Hard Blasters Crew (HBC).

Akifunguka kupitia The Playlist ya Times FM, rapa huyo mkongwe aliyechonga barabara kwa wasanii wengi wa rap nchini, amesema kuwa wakati wanaandaa albam zao na HBC, hawakuwa na kitu mfukoni kiasi cha kufikia hatua ya kunywa maji ya bomba lililokuwa chooni ili waendelee kufanya kazi yao studio.

“Nakumbuka wakati huo tunarekodi, unaenda kunywa maji chooni hivi… kwenye bomba liliko chooni unakula na mihogo yako ili uweze ku -buy time ya kuendelea kuwa studio siku nzima. Kwamba hakuna hata pesa ya kula chips mzee,” Profesa alifunguka.

Mkali huyo wa rap mwenye majina mengi ya kupewa kwa kuwa mbabe wa kurap, alieleza kuwa wakati wamepata nafasi ya kurekodi albam yao kama HBC, kuna wakati akiwa anafanya kazi Tanga, ilimlazimu kupanda malori ya mizigo usiku ili arejee kazini Jumapili usiku, kwani muda wa usiku aliokuwa akimaliza kurekodi jijini Dar es Salaam, magari ya abiria hayakuwepo.

Katika hatua nyingine, Profesa Jay alieleza tukio la kurekodi wimbo wake wa ‘Jina Langu’ katika studio za Bongo Records chini ya mtayarishaji nguli, P-Funk Majani. Alisema alimshangaza Majani kwani alikuwa akisikia mara kadhaa mdundo wa wimbo huo, ndipo alipomuomba mtayarishaji huyo aingize sauti.

Alisema baada ya kuwekewa mdundo, alipita na mashairi yote matatu bila kukwama, kitu ambacho kilimshangaza Majani pamoja na ukubwa wa mashairi yaliyowekwa ndani.

Profesa amewashauri wasanii wa Tanzania kuendelea kuandika vitu ambavyo vinagusa jamii na kuitangaza Tanzania kwa maslahi ya taifa kwa ujumla.

Hivi karibuni, aliachia wimbo wake ‘Pagamisa’ akiwa na mtayarishaji wa muziki, Mr. T-Touch.
Read More

Polisi 458 Wafukuzwa Kazi

Jumla ya maofisa wa Jeshi la Polisi wapatao 458 wamefukuzwa kazi kutokana na utovu wa nidhamu kuanzia mwaka 2015 hadi Machi mwaka huu.

Kauli hiyo imetolewa jana Aprili 7 na Mkuu wa Jeshi la Polisi IGP Simon Sirro alipokuwa akizungumza mbele ya Rais John Magufuli wakati wa uzinduzi wa nyumba 31 za Polisi na ufunguzi wa kituo cha Polisi cha Utalii na Kidiplomasia jijini Arusha.

Sirro alisema kazi ya Jeshi la Polisi ni kurekebisha mienendo ya wananchi, hivyo kabla hawajawaelimisha wananchi wanapaswa kuwa na mienendo mizuri wao kwanza.

Alifafanua kwa kulitambua hilo ndiyo maana askari waliokwenda kinyume na azma hiyo walichukuliwa hatua ikiwa ni pamoja na kufukuzwa kazi, ambapo kwa mwaka 2015, 198 walifukuzwa kazi.

Alisema kwa mwaka 2016 walifukuzwa askari 165, 2017 (81) na kuanzia Januari hadi Machi mwaka huu wamefukuzwa askari 14.

“Hatuna muhali kuwachukulia hatua askari wanaokiuka utaratibu na nidhamu ya utendaji katika Jeshi la Polisi,” alisema IGP Sirro.
Read More

Baba Mzazi: 'Abdul Nondo babu yake ni muasisi wa TANU'

Abdul Nondo, mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) ambaye anakabiliwa na kesi ya kujiteka mwenyewe, mzazi wake Omar amethibitisha kuwa baba yake alizaliwa mwaka 1919 huko Ujiji, Kigoma na kuwa ni miongoni mwa waasisi wa chama cha Tanu.

Mzee Omar, alisema baba yake huyo aliyemtaja kwa jina la Omar Kagobe alipata watoto 30, mmoja akiwa yeye.

“Nashangaa hao wanaomkamata na kumhoji mtoto wangu kuwa sio raia, wananichekesha sana kwa kuwa najua mwisho wa siku watajua ukweli wake. Ukweli ni kwamba wazazi wangu ndio waasisi wa Tanu na walishiriki kikamilifu katika kupigania uhuru wa nchi hii, hivyo suala hilo halinipi wasiwasi wala hofu na hivyo vyeti wanavyovitaka mbona vipo tu, ila waelewe kuwa sisi ni Wamanyema halisi na ni raia halali wa nchi hii,” alisema.

Naye Mwenyekiti wa ACT - Wazalendo, Mkoa wa Kigoma, Sendwe Mbaruku, alitoa taarifa Alhamisi kuhusu suala la Nondo kuhojiwa na uhamiaji na kusema; “Kijana Abdul ni mtoto wetu hapa Kigoma, wazazi wake ni wakazi na wapiga kura wa hapa Ujiji, zaidi ni Watanzania wenzetu.”

Maelezo haya yametolewa na mzazi huyo Siku chache baada ya Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP), Abdul Nondo kuhojiwa na Idara ya Uhamiaji Mkoa wa Dar es Salaam kuhusu uraia wake.

Mzazi huyo amesema babu yake Nondo, alishawahi kuwa Polisi kwa miaka 18 kuanzia mwaka 1940 hadi 1958 na alishafanya kazi huko Mabatini mkoani Mwanza na sehemu nyingine za nchi.

Alisema babu yake wakati akiwa polisi, ndipo zilipoanzishwa Kota za Msimbazi, Dar es Salaam na jina lake lilikuwa maarufu, akijulikana kama Mzee Kagobe.

Kama haitoshi alisema bibi yake Nondo alikwenda kuhiji, mnamo 1970 na alipewa hati ya kusafiria ya Tanzania, huku akihoji, “Kama angekuwa sio raia wa Tanzania angepewaje hati hiyo?”

Baada ya Nondo kuripoti polisi mjini Mafinga alishikiliwa na jeshi hilo Mkoa wa Iringa na baadaye kukabidhiwa kwa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam.

Kamanda wa kanda hiyo, Lazaro Mambosasa alisema kupitia uchunguzi wa kisayansi, wamebaini kuwa hakuwa ametekwa, bali alijiteka na tayari suala lake lipo mahakamani, Iringa.
Read More

Mbunge Mchafu aitaka Serikali kupitia Sheria upya

Wakati Wabunge walikuwa wakichangia mapendekezo yao katika  bajeti ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2018/19   Mbunge wa viti maalum CCM Hawa Mchafu Chakoma  ameishauri serikali kuanzisha namna bora ya  mpango wa pensheni kwa wazee waliolitumikia taifa.

Hawa Mchafu alisema ;"Nashindwa kufahamu mfuko wa moja kwa moja ambao upo kwa ajili ya wazee, muda umefika sasa ule mchakato wa pensheni kwa wazee uje sasa ili kuweza kuwasaidia wazee wa taifa letu ambao kwa nafasi zao walisaidia sana nchi yetu”

“Niipongeze Serikali pia kwa kuanzisha miradi mbalimbali mikubwa ikiwemo ujenzi wa bomba la mafuta, ujenzi wa viwanja vya ndege n.k  ....ni wazi itaambatana na upatikanaji wa ajira lakini niishauri Serikali ihakikishe inafuatilia mikataba ya kazi kwa watanzania inayofanyika katika miradi hiyo kwamaana kumekuwa na ukakasi mkubwa sana mikataba mingi inaukiukwaji wa kisheria” –Hawa Mchafu
Read More

Mwanamke wa Kwanza Kupata Degree Tanzania Atunukiwa Tuzo

Dkt Maria Kamm ndiye  mwanamke wa kwanza wa Tanzania kupata Shahada ya kwanza (Degree) na jana ametunukiwa tuzo ya heshima katika tuzo za Malkia wa Nguvu zinazoandaliwa na Clouds Media.

Mama Kamm ambaye aliwahi kuwa Mkuu wa Shule ya Sekondari ya Weruweru iliyopo Mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro, akiwa kama Mzalendo wa kweli, ametumia maisha yake kwa kiasi kikubwa kuwashauri na kuwaelimisha vijana katika masuala mbalimbali ya Taifa.

Mgeni Rasmi katika utoaji wa Tuzo hizo uliofanyika katika Ukumbi wa Mikutano wa Mwl Nyerere Posta jijini Dar, alikuwa Waziri wa  Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dr. Ummy Ally Mwalimu.
Read More

Serikali Yapata Mkopo Wa Shilingi Bilioni 34 Kutoka Mfuko Wa Maendeleo Ya Kiuchumi Wa Kuwait

Na Benny Mwaipaja, WFM, Dodoma
Serikali ya Kuwait kupitia Mfuko wa Maendeleo wa Kiuchumi wa Kuwait (Kuwait for Arab Economic Development Fund), na Serikali ya Tanzania zimetiliana saini  rasimu ya mkataba wa  kuipatia Tanzania mkopo wenye masharti nafuu wa dola milioni 15.3, sawa na zaidi ya shilingi bilioni 34, kwa ajili ya mradi wa  kilimo cha umwagiliaji katika Bonde la Luiche, mkoani Kigoma,  lenye ukubwa wa  hekta 3,000.

Rasimu hiyo ya Mkataba imesainiwa na Kiongozi wa ujumbe wa wataalamu na Mshauri wa Masuala ya Kilimo wa Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait,  Dkt. Abdulrida Bahman na  kwa upande wa Tanzania ikisainiwa na Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. Khatibu Kazungu, mjini Dodoma.

Waziri wa Fedha na Mipango Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango (Mb)  amesema hatua hiyo imfikiwa baada ya timu ya wataalamu kutoka Kuwait kutembelea eneo la mradi mkoani Kigoma na kuridhishwa na umuhimu wake kiuchumi kwa wananchi wa mkoa huo na taifa kwa ujumla.

 “Mradi huo una umuhimu mkubwa kwa watanzania kwa kuwa wataweza kuwa na kilimo cha umwagiliaji cha Mpunga na Mbogamboga kwa mwaka mzima badala ya kilimo cha msimu cha kutegemea mvua, na katika siku zijazo Kigoma itakua miongoni mwa mikoa inayozalisha mchele kwa wingi”, alisema Dkt. Mpango.

Dkt. Mpango amesema kuwa Serikali ya Tanzania na Kuwait zitatia saini mkataba rasmi wa mkopo huo wenye masharti nafuu ifikapo mwishoni mwa mwezi Juni mwaka huu ili mradi huo uanze kutekelezwa ili kuongeza kipato cha wananchi na  kuwa na uhakika wa chakula.

Amesema Nchi ya Kuwait imekuwa ikiisaidia Tanzania katika kutekeleza miradi mbalimbali ikiwemo ya ukarabati wa Hospitali ya Mnazi mmoja, Zanzibar kwa kiasi cha dola za Marekani milioni 13.6 sawa na shilingi bilioni 31.

"Kwa upande wa Tanzania Bara wametoa mkopo nafuu wa shiingi bilioni 115 kwa ajili ya kuboresha barabara ya Chaya hadi Nyahua (km 85) kwa kiwango cha lami ambayo ni muhimu kwa kuwa inaunganisha mikoa ya Magharibi mwa Tanzania" aliongeza Dkt. Mpango

Miradi mingine ambayo  nchi hiyo imeonesha nia ya kuisaidia nchi, ni pamoja na ujenzi wa jengo la abiria katika Uwanja wa Ndege wa Mwanza, uboreshaji wa barabara ya kutoka Morogoro hadi Dodoma na ujenzi wa barabara za mzunguko za kuingia na kutoka mjini Dodoma ambazo zitasaidia kuondoa msongamano wa magari yanayopita katikati ya mji huo kutokana na kuongezeka kwa idadi ya watu na vyombo vya moto baada ya Makao Makuu ya Serikali kuhamia Dodoma.

Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Mpango ameishukuru nchi ya Kuwait kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait, kwa nia yake njema na thabiti katika kusaidia nchi ya Tanzania kutekeleza kwa mafanikio miradi ya Maendeleo ya kiuchumi katika nia yake ya kupata maendeleo Stahiki.

Kwa upande wake Kiongozi wa ujumbe wa wataalamu na Mshauri wa Masuala ya Kilimo wa Mfuko wa Maendeleo ya Kiuchumi wa Kuwait, Dkt. Abdulrida Bahman, ameishukuru Serikali ya Tanzania kupitia Waziri wa Fedha na Mipango kwa ukarimu pamoja na Idara ya Taifa ya Umwagiliaji kwa ushirikiano mzuri katika hatua za kufanikisha utekelezaji wa mradi wa umwagiliaji  wa Bonde la Luiche, Mkoani Kigoma.

“Tumetembelea eneo la mradi kwa takribani wiki mbili tumejionea uzuri wa nchi hii na fursa zilizopo, hii ni nchi tajiri na inaweza kuwa tajiri kuliko Kuwait kwa kuwa kila kitu kinachoweza kufanya nchi hii iwe tajiri kipo”.Alieleza Dkt. Bahman.

Amesema mradi huo wa umwagiliaji hautakuwa wa mwisho kupewa fedha na mfuko huo bali utaendelea kusaidia kutekeleza miradi mingine mingi kama ilivyokuwa ikifanya, kutokana na ushirikiano mzuri, wa kihistoria, na wa muda mrefu kati ya nchi hizo mbili.

Mwisho.
Read More

Habari Zilizopo Katika Magazeti ya Leo Jumapili ya Apriil 8



Read More

Rais Magufuli atangaza ajira mpya 1500 Polisi....Pia Kawapa Bilioni 10

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli  tarehe 07 Aprili, 2018 ameungana na Watanzania wote kuadhimisha siku ya mmoja wa waasisi wa Taifa Hayati Sheikh Abeid Amani Karume, Rais wa Kwanza wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Kwanza wa Baraza la Mapinduzi kwa kuzindua kituo cha polisi, kufungua nyumba 31 za askari polisi na kushuhudia maonesho ya Polisi katika uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Amri Abeid Jijini la Arusha.

Kituo cha polisi cha watalii na wanadiplomasia kilichopo Naura, kituo cha polisi cha Muriet, na nyumba za 18 kati ya 31 za makazi ya polisi vimejengwa kwa mchango wa wafanyabiashara wa Mkoa wa Arusha  na Benki ya CRDB kwa gharama ya Shilingi Milioni 753, wakati nyumba za polisi 13 zimejengwa na Serikali kwa gharama ya Shilingi Milioni 250.

Mhe. Rais Magufuli aliagiza kujengwa kwa nyumba hizo baada ya kutokea ajali ya moto iliyosababisha nyumba 13 za makazi ya askari polisi na mali zao kuungua moto tarehe 27 Septemba, 2017.

Katika kutekeleza agiza hilo Mkuu wa Mkoa wa Arusha Bw. Mrisho Gambo akaamua kuwashirikisha wafanyabiashara na benki ya CRDB kuchangia ujenzi huo na kufanikiwa kujenga nyumba nyingine 18 na vituo hivyo viwili vya polisi.

Pamoja na kuzindua miradi hiyo Mhe. Rais Magufuli ameshuhudia maonesho ya Jeshi la Polisi ya kuzuia na kupambana na uhalifu yakiwemo kukabiliana na waandamanaji haramu, wezi, waporaji watumiao silaha na magaidi, yaliyofanyika katika uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Amri Abeid.

Akizungumza baada ya maonesho hayo Mhe. Rais Magufuli amesema Taifa litaendelea kumkumbuka Hayati Sheikh Abeid Amani Karume kwa juhudi zake za kujenga nchi ikiwemo kuwajengea makazi wananchi masikini kule Zanzibar na ametoa wito kwa Watanzania kumuenzi kwa kudumisha amani na kuchapa kazi.

Pamoja na kumpongeza Mkuu wa Mkoa wa Arusha Bw. Mrisho Gambo kwa jitihada zake za kuwaunganisha wadau na kisha kufanikiwa kujenga nyumba za askari na vituo vya polisi Mhe. Rais Magufuli ametoa Shilingi Bilioni 10 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za askari polisi wa vyeo vya chini nchini, na amewaagiza viongozi wa mikoa yote kuwashirikisha wadau katika ujenzi huo kama ilivyofanyika mkoani Arusha ili kukabiliana na tatizo la askari kukosa nyumba za makazi.

“Askari polisi mnafanya kazi kubwa sana ya kulinda raia na mali zao, natambua juhudi kubwa mnazofanya na napenda kuwashukuru sana, naomba Watanzania wote tuendelee kuliunga mkono Jeshi la Polisi.

“Wakati naingia madarakani kulikuwa na mauaji kila wakati, kule Kibiti pekee yake waliuawa watu 59 wakiwemo askari polisi 17 na raia 42, Jeshi la Polisi limefanya kazi kubwa na sasa mauaji yale yamedhibitiwa, ni lazima tulipongeze jeshi letu” amesema Mhe. Rais Magufuli.

Aidha, Mhe. Rais Magufuli amekubali maombi ya Mkuu wa Jeshi la Polisi IGP Simon Sirro la kuongezewa idadi ya askari na kupandishwa vyeo kwa maafisa wa polisi ambapo ameruhusu Jeshi la Polisi kuajiri askari wapya 1,500 kutoka Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na kumpelekea mapendekezo ya maafisa wanaostahili kupandishwa vyeo.

Mhe. Rais Magufuli amempongeza IGP Sirro kwa hatua ya kuwafukuza kazi askari polisi 458 waliokutwa na makosa ya kinidhamu na uadilifu kuanzia mwaka 2015 hadi sasa, na ametaka hatua hizo ziendelee kuchukuliwa dhidi ya askari wengine wanaokiuka maadili na taratibu za kazi ili kuondoa malalamiko kutoka kwa wananchi yakiwemo upokeaji rushwa na unyanyasaji raia kwa kuwabambikiza kesi.

Halikadhalika Mhe. Rais Magufuli amepiga marufuku askari, maafisa wa polisi na viongozi wengine wa Serikali kushiriki ufyekaji wa mashamba ya bangi na badala yake ametaka mashamba hayo yanapobainika yafyekwe na wanavijiji wenyewe waliohusika kuyalima.

Maadhimisho hayo yamehudhuriwa na Mke wa Rais Mhe. Mama Janeth Magufuli na viongozi mbalimbali wakiwemo Mawaziri, Naibu Mawaziri, viongozi wakuu wa vyombo vya ulinzi na usalama, wabunge na wananchi.

Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Arusha
07 Aprili, 2018
Read More

Waziri Ndalichako atoa agizo kwa shule binafsi


Serikali imewataka wamiliki wa shule binafsi nchini kutumia ujuzi na uzoefu wao katika nyanja ya elimu ili kuishauri Serikali nini cha kufanya ili kiwango cha elimu inayotolewa hapa nchini kuendelea kukua.


Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa JOYCE NDALICHAKO amesema hayo Mjini Dodoma alipokuwa akifungua mkutano wa Chama cha Wamiliki wa shule binafsi na kuongeza kuwa ni jukumu la jamii nzima kuhakikisha elimu nchini inakuwa.
Nao baadhi ya wamiliki wa shule binafsi wamesema kuna mambo mengi ambayo Serikali inaweza kujifunza kutoka katika shule hizo na kuzifanya shule za Serikali ziwe zinafanya vizuri katika mit i hani ya kitaifa kama zilivyo za binafsi.
Mkutano wa siku moja umeshirikisha wamiliki wa shule binafsi kutoka nchi nzima, lengo kuu likiwa ni kuangalia mafanikio na matatizo ambayo shule binafsi nchini zinakabiliwa nazo.
Read More

Kauli ya Humphrey Polepole Baada ya Askofu Kakobe Kuitwa na Idara ya Uhamiaji

Baada ya watu mbalimbali kutoa maoni yao juu ya kuitwa kwa Askofu Kakobe na idara ya Uhamiaji kuhojiwa Uraia wake, Katibu wa Itikadi na Uenezi CCM Humphrey Polepole ameandika yafuatayo kwenye ukurasa wake wa Twitter; “Mbona kuhojiwa jambo la kawaida? baadhi ya watu wanajenga tabia ya hovyo sana”

“Watu “wakubwa” wakiitwa kuhojiwa inaonekana kitu cha ajabu. Mbona huku mtaani kuhojiwa Polisi ni kitu cha kawaida tu, tuanze kuzoea na hasa ktk awamu ya 5 kwamba, na tunasisitiza binadamu wote ni sawa” 
Read More

Tazama live: Man city vs Man United leo april 7

Read More

Marekani yatangaza vikwazo dhidi ya Warusi 38 na makampuni ya Urusi

Ikulu ya Marekani, White House imetangaza vikwazo dhidi ya Warusi 38 na makampuni, ikisema Marekani inakabiliana na kile kinachoendelea ikiwa ni mbinu za Serikali ya Urusi  za “vitendo vya kuvuruga” demokrasia nchi za Magharibi na ulimwenguni kote.

Katika muhtasari alioutoa msemaji wa White House Sarah Huckabee Sanders Ijumaa amesema Marekani bado inataka kushirikiana naUrusi

“Pia, kile tunachotaka kukiona ni serikali ya Urusi ibadilishe mwenendo wake kikamilifu. Tunataka kuendelea kuwa na mazungumzo na kufanya kazi siku za usoni kwa kujenga mahusiano mazuri,” Sanders amesema.

Vikwazo hivyo vitawekwa dhidi ya makampuni saba ya Urusi – ikiwemo Oleg Deripaska, kampuni ya aluminium ambayo ni mshirika wa karibu na Rais Vladimir Putin- na makampuni mengine 12 ambayo wanayamiliki au kuyahodhi.

Pia maafisa 17 wa serikali ya Urusi, na kampuni ya kutengeneza silaha inayomilikiwa na serikali ya Urusi na kampuni zake tanzu, benki ya Urusi, pia zitalengwa na vikwazo hivyo.
Read More

Askofu Mkuu Zachary Kakobe aitwa Uhamiaji Jumatatu kuhojiwa juu ya uraia wake

Ofisi ya Uhamiaji Mkoa wa Dar-Es-Salaam, imemwandikia barua Askofu Mkuu wa Kanisa la Full Gospel Bible Fellowship (FGBF), Askofu Zachary Kakobe, kumwita kwa ajili ya mahojiano.

 Askofu Kakobe ametakiwa kufika katika ofisi hiyo, Jumatatu 9.4.2018 saa 4 asubuhi, na kuonana na Afisa Uhamiaji wa Mkoa wa Dar-Es-Salaam, ili kuhojiwa juu ya uraia wake.

Alipoulizwa kwa njia ya simu, Askofu Kakobe amethibitisha kupokea barua hiyo, na kusema kifupi tu kwamba, atakwenda kwenye mahojiano hayo.

Tukio hili linakuja baada ya sekeseke kati ya Askofu huyo na TRA, kuhitimishwa tarehe 20.2.2018, siku ambayo Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Charles Kichere, alipotoa taarifa kwa umma juu ya uchunguzi wao; na baadaye kusema mjadala huo umefungwa.
Read More

RC Gambo Amtoa Hofu Rais Magufuli Kuhusu Maandamano ya Mange Kimambi

Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mrisho gambo amemtaka Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli kutotishwa na maandamano ya mitandaoni yanayoratibiwa na Mange Kimambi, kwani mkoa wa Arusha uko salama.

Mrisho Gambo ameyasema hayo leo alipokuwa akitoa salam zake kwa Rais Magufuli, kwenye sherehe za uzinduzi wa nyumba za polisi mkoani Arusha, kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abedi.

Kwenye salamu hizo Mrisho Gambo amesema mkoa wa Arusha ni salama na wakazi wa Arusha hawana haja ya maandamano, kwani wanachohitaji ni uongozi wake ambao unawaletea maendeleo makubwa.

Mrisho gambo aliendelea kwa kueleza kuwa anatambua kazi ya kubwa aliyonayo Rais ya kupigana vita ya uchumi, na watu wengi wasiopenda nchi hii watachukia kutokana na hilo.

“Mheshimiwa Rais nikuhakikishie tu Arusha ni salama, wala usitishwe na mbwembwe za kwenye mitandao, watanzania halisi ni hawa hapa wenye Arusha yao. 
"Watanzania wa Arusha wamechoka na maandamano, wanataka uongozi wa kwako ambao unawaletea maendeleo. Ninajua vita uliyokuwa nayo ni kubwa sana, Mwl. Nyerere alikuwa na vita ya ukombozi, akaimaliza salama, 
"Mheshimiwa Rais vita yako wewe ni ya kiuchumi, ni vita inayopigana na mabeberu ambao wanawatumia wengine kukwamisha jitihada zako. Watu wengi ambao hawaitakii mema nchi hii hawawezi kuipenda”, amesema Mrisho Gambo.

Sambamba na hilo Mkuu wa mkoa huyo wa Arusha amemshukuru Rais Magufuli na wadau kwa kufanikisha ujenzi wa nyumba hizo za askari polisi, ambazo awali ziliteketea kwa moto.
Read More

Rais Magufuli Awapiga Marufuku Polisi Kufyeka Mashamba ya Bangi

RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amewataka maofisa wa Jeshi la Polisi na Makamishna wake kutoyafyeka na kuyachoma moto mashamba ya bhangi na badala yake watumie njia za kiintelijensia kuwababini watuhumiwa, kuwakamata na kuwashughulikia ikiwa ni pamoja na kuwafikisha katika vyombo vya sheria.

Rais ameyasema hayo leo wakati akiwahutubia wananchi wa Arusha katika Uwanja wa Amri Abeid baada ya kuzindua kituo cha polisi na nyumba za polisi mkoani humo.

“Hakuna kitu kinachonikera kama Askari Polisi kwenda kufyeka mashamba ya bhangi, makamanda wako na askari wako, wasikate mashamba ya bangi, hawakuajiriwa kufyeka bhangi. Niwashauri tu kwamba, tumieni njia za kintelijensia, mtawashika tu, kama shamba lipo karibu na kijiji, kamata kijiji kizima, wazee, vijana, wanawake hata na watoto, ndio wakafyeke hilo shamba la bhangi.

“Nasema askari wasiende kufyeka bhangi, hawakuajiriwa kufyeka bhangi, usiwatume askari wako kufyeka bhangi, wataumwa nyoka bure, wamevaa uniform nzuri, msidhalilishe jeshi kwa kufyeka bhangi, mimi nisingefyeka bhangi na wa kufyeka wapo.

“Nilimuona Waziri naye yumo anafyeka na kuchoma moto shamba la bhangi, juzi nikaona tena RPC wa Dodoma naye anafyeka shamba la bhangi na askari wake, mpaka akachoka anasema hili shamba lililobaki tutalimalizia kesho. Inashangaza sana, tusijidhalilishe hivyo,” alisema Magufuli.

Aidha, Rais Magufuli amelitaka Jeshi la Polisi na vyombo vingine vya Usalama kuendelea kuimarisha hali ya amani nchini na kuwatumikia Watanzania kwa maendeleo ya Taifa.
Read More

Rais Magufuli awapa rungu polisi

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, amewataka jeshi la polisi kufanya lolote lililopo ndani ya uwezo wao, ili kuhakikisha mani ya nchi haivunjwi na kubaki na utulivu.

Kauli hiiyo imetolewa leo jijini Arusha alipokuwa akihutubia kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, na kusema kwamba anatambua kazi ya jeshi la polisi ingawa kuna watu ambao wana wabeza, hivyo wasiyumbishwe na watu hao, ila waendelee kuchapa kazi kwani yeye kama Amiri Jeshi Mkuu wao yuko pamoja nao.

“Kuna watanzania wanaongea maneno ya kebehi kebehi kuhusu polisi, hawajui thamani ya polisi, ndugu zangu polisi tembeeni kifua mbele, na kwa bahati nzuri mimi ni shemeji yenu, mkwe wenu, msiwe na wasi wasi, maneno ya kashfa na kebehi yanayozungumzwa na wengine wala yasiwakatishe tamaa. 
"Nilipopewa urais nikaapa kuhakikisha nchi inakuwa salama, na kuhakikisha nchi inakuwa salama, lazima jeshi la polisi liwe salama, endeleeni kuilinda amani ya nchi yetu, mtakayoyaamua yaamueni na mimi nitawasapoti, niliapa kuilinda amani ya nchi hii kwa nguvu zote na nitailinda”, amesema Rais Magufuli.

Sambamba na hilo Rais Magufuli amesema anatambua mazingira magumu waliyonayo askari polisi hususan wa vyeo vya chini, hivyo atahakikisha anatatua kero zao ikiwemo kuboresha makazi yao.
Read More

IGP Sirro atoa maelekezo kwa wanaotaka kuandamana

Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP) Simon Sirro amesema Jeshi lake liko imara kweli kweli katika kupambana na watu wanaotaka kuleta uvunjifu wa amani nchini, huku akiwasii wanaotaka kuandamana kuacha mara moja kwani kitakachowapata wasije kulaumiana

IGP Sirro ametoa kauli hiyo leo (Aprili 7, 2018) wakati akitoa salamu zake kwa Rais Dkt. Magufuli katika uwanja wa Sheikh Amri Abeid uliopo mjini Arusha baada ya uzinduzi wa nyumba za askari na kushuhudia maonesho ya utayari ya jeshi hilo katika kukabiliana na uhalifu.

"Mhe. Rais Magufuli Jeshi lako la  Polisi liko imara tena imara kweli kweli, kwa kupambana na watu wote wanaotaka kuleta uvunjifu wa amani hapa nchini na kwa bahati nzuri wananchi wapo pamoja na wewe Rais na Jeshi lako.
" Ila naomba nitoe ushauri wa bure kwa wale wote wenye nia ya kuchafua amani ya nchi yetu , ni wasii waache mara moja na kama wataona ushauri huo hauna maana basi baadae tusilaumiane", amesema IGP Sirro.

Pamoja na hayo, IGP Sirro ameendelea kwa kusema "upo uhamasishaji kwenye mitandao, na hili niseme  naamini wameshaandamana kwenye mitandao na wameshamaliza maandamano yao. Kwa hiyo la msingi sana tujenge nchi yetu".

Kwa upande mwingine, IGP Sirro amesema katika kipindi cha mwezi Januari hadi Februari mwaka 2018 kuna jumla ya matukio ya jinai yaliyoripotiwa ni 96,363 ikilinganishwa na matukio 104,073 yaliyoripotiwa kipindi kama hicho mwaka 2017.
Read More

KIKOSI CHA YANGA KITAKACHO WAVAA WAETHIOPIA HIKI HAPA, KAMUSOKO KUANZA LEO

Kikosi cha Yanga kitakachoanza dhidi ya Welaytd Dicha FC, mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika


1. Youthe Rostand
2. Hassan Kessy
3. Mwinyi Haji
4. Abdallah Shaibu
5. Andrew Vincent
6. Thaban Kamusoko
7. Yusuph Mhilu
8. Raphael Daud
9. Pius Buswita
10 Ibrahim Ajibu
11. Emmanuel Martin

Kikosi cha akiba

12. Ramadhan Kabwili
13. Juma Abdul
14. Nadri Haroub
15. Patto Ngonyani
16. Juma Mahadhi
17. Yohana Mkomola
18 Geoffrey Mwashiuya
Read More

KAMUSOKO ANAWASUBIRI KWA HAMU WAETHIOPIA JIONI

Kiungo wa Yanga, Thabani Kamusoko amewapia wapinzani wao Wolayta Dicha wa Ethiopia katika mchezo wao wa leo kwa kusema wamejiandaa vilivyo kuwafunga.


Yanga leo Jumamosi inacheza na Dicha katika mechi ya kuwania kufuzu hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho baada ya kutolewa katika Ligi ya Mabingwa. Kamusoko raia wa Zimbabwe na wachezaji wenzake wamepania kuifunga Dicha katika mchezo huu wa kwanza wa mtoano wa Kombe la Shirikisho.

Kama Yanga itaitoa Dicha na kutinga makundi kwenye michuano hiyo, itakuwa ni mara ya pili ndani ya misimu mitatu kwani katika msimu wa 2015/16, timu hiyo iliishia kwenye hatua hiyo.

Akizungumzia maandalizi yao kuelekea mchezo huo wa leo, Kamusoko alisema: “Michuano ya Caf ukiangalia ni migumu na ina mazingira magumu sana ya kusonga mbele kutokana na jinsi ilivyo.

“Ukiangalia kwa hatua hii tuliyofikia timu ikicheza mechi mbili na kushinda basi inaingia makundi, kitu hicho usichukulie rahisi, unatakiwa kufanya kazi kweli.

“Sisi tumejiandaa vizuri na tunawajua wapinzani wetu wapo vipi, tunajipanga kufanya vizuri kuhakikisha tunaingia tena hatua ya makundi.

“Tunawaomba mashabiki wetu waje kwa wingi kuisapoti timu yao kwa sababu wasipoisapoti itakuwa ngumu kwetu kufanya vizuri kwani tunajiona kama tunachokifanya si kizuri na hakiwapendezi wao mashabiki.”

CHANZO: CHAMPIONI
Read More

Taharuki Shinyanga : ALIYEVAA KIASKOFU NA KUSHIKILIA BIBLIA ,MAJEMBE AZUIA MAGARI BARABARANI,TAZAMA PICHA

Taharuki ya aina yake imetokea katika eneo la Sisi kwa Sisi ‘Ushirika’ barabara ya Shinyanga kwenda Mwanza mjini Shinyanga baada ya mwanaume ambaye hajajulikana jina wala makazi yake aliyevaa nguo nyekundu za kiaskofu akiwa amebeba silaha za jadi kusimamisha magari barabarani.

Tukio hilo lililodumu kwa takribani dakika 45 limetokea leo Jumamosi Aprili 7,2018 saa tano asubuhi.

Mwanaume huyo anayekadiriwa kuwa na miaka zaidi ya 40 alikuwa amevaa nguo nyekundu,kofia nyekundu yenye msalaba,biblia,mito,midoli,msumeno,baiskeli na majembe yenye mipini ya nondo.

Mashuhuda wa tukio hilo wameiambia Malunde1 blog kuwa jamaa huyo alifika katika eneo la Ushirika karibu na ofisi za halmashauri ya wilaya ya Shinyanga kisha kusimama kwenye eneo la kuvukia ‘Zebra’ akaanza kusimamisha magari.

“Alifika hapa akiwa amevaa joho jekundu la kiaskofu pamoja na kofia nyekundu yenye msalaba huku akiwa ameshikilia biblia,baiskeli,msumeno na majembe,akatandaza barabarani vitu alivyokuwa navyo akawa anasimamisha magari huku akisema yeye ni Malkia wa Nguvu ametumwa na Mungu kuja Kukomboa nchi ya Tanzania,wameeleza mashuhuda wa tukio hilo.

Aidha wamesema wakati akisimamisha magari alisikika akisema bado usiku ,hapajakucha wasiendelee na safari na kwamba yeye ametumwa kuja kukomboa nchi.

“Alisimamisha kila gari pande zote mbili,akasababisha foleni ndefu,dereva wa basi la Mgamba lililokuwa linatoka Mwanza alipogoma kusimama ndipo jamaa akapasua kioo cha mbele akitumia majembe yake ambayo yamechomelewa nondo”,waliongeza mashuhuda.

Kufuatia taharuki hiyo jeshi la polisi lilifika eneo la tukio na kumkamata mwanaume huyo ambaye alionekana kutokuwa na wasiwasi wowote akisema wampeleke tu kwenye vyombo vya sheria kwani yeye hana kosa bali amekuja kukomboa nchi.

Hata hivyo inaelezwa kuwa jana jamaa huyo ambaye hajulikani ametokea wapi alionekana eneo la Ushirika akiwa amevaa kanzu nyeupe na kofia 'kibaraghashia' na hata juzi alifika katika ofisi za halmashauri ya wilaya ya Shinyanga zilizopo hapo Ushirika.

Mwanaume aliyevaa nguo nyekundu baada ya kuvua joho jekundu akiwa amesimama katika eneo la kuvukia Zebra eneo la Ushirika barabara ya Shinyanga - Mwanza baada ya kuvua joho lake jekundu na kubakiza tisheti na kaptura nyekundu . Pichani ni vifaa alivyokuwa navyo ikiwemo baiskeli,mfuko mwekundu,biblia,midoli,biblia na nguo nyekundu -Picha na Malunde1 blog
Jamaa akichezea mdoli barabarani
Mwanaume huyo akiwa ameshikilia msumeno na jembe akizuia magari yasipite
Jamaa akisimamisha magari
Jamaa akisimamisha mabasi
Jamaa akisimamisha basi
Askari polisi wakimwondoa barabarani jamaa huyo akiwa amevaa nguo nyekundu na kofia yenye msalaba
Askari polisi akiokota vifaa vya jamaa huyo ambavyo ni biblia,mto,nguo na mdoli
Askari polisi akiwa ameshikilia majembe ya jamaa huyo
Askari polisi akiruhusu magari yaendelee na safari
Mwanaume huyo akiwa chini ya ulinzi wa polisi baada ya kuondolewa barabarani.Nguo nyekundu hapo chini ni joho lake la kiaskofu alilolivua baada ya kuanza kusimamisha magari
Mwanaume huyo akiwa chini ya ulinzi wa polisi 
Mwanaume huyo akipelekwa kwenye gari la polisi
Askari polisi wakimpeleka jamaa huyo kwenye gari la polisi
Mwanaume huyo akipelekwa kwenye gari la polisi
Jamaa akipanda kwenye gari la polisi
Askari polisi akiwa ameshikilia msumeno na majembe mawili ya mwanaume huyo
Jamaa akiwa kwenye gari la polisi
Wananchi wakishuhudia tukio hilo
Mwanaume huyo akiondoka na polisi
Read More
Powered by Blogger.

Hot

© Copyright KAHAMA 24